KABUDI AANZA KAZI RASMI MOCLA
Waziri wa Katiba na Sheria,
Mhe. Prof. Palamagamba Kabudi (Mb) akiongea na watumishi wa Wizara hiyo mara baada
ya kupokelewa kuanza majukumu rasmi ya kuongoza Wizara hiyo, tarehe 20 Agosti,
2024 Mtumba Dodoma.
Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Prof. Palamagamba Kabudi (Mb) akipokea nyaraka mbalimbali za utendaji kazi kutoka kwa aliyekuwa Waziri wa Wizara hiyo ambaye sasa ni Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Balozi Dkt. Pindi Chana (Mb) wakati wa makabidhiano ya Ofisi yaliyofanyika Ofisi za Wizara Mtumba, jijini Dodoma, tarehe 20 Agosti, 2024.
Waziri wa Katiba na Sheria
Mhe. Prof. Palamagamba Kabudi (Mb) akiwa na Waziri wa Maliasili na Utalii
Mhe. Balozi Dkt. Pindi Chana (Mb) wakisaini nyaraka za makabidhiano ya ofisi
katika Ofisi za Wizara ya Katiba na Sheria leo Agosti 20, 2024
Mtumba jijini Dodoma.
Waziri wa Katiba na Sheria
Mhe. Prof. Palamagamba Kabudi (Mb.) akisaini kitabu mara baada
ya kuwasili Ofisi za Wizara Mtumba, jijini Dodoma kwa ajili ya hafla ya
makabidhiano ya Ofisi tarehe 20 Agosti, 2024.
Naibu Waziri Wizara ya Katiba
na Sheria Mhe. Jumanne Sagini (wa kwanza kulia) akiwa pamoja na Katibu Mkuu wa
Wizara Bw. Eliakim Maswi (wa kwanza kushoto) wamewaongoza Watumishi wa Wizara
ya Katiba na Sheria katika mapokezi ya Naibu Katibu Mkuu mpya wa Wizara
hiyo Dkt. Franklin Rwezimula tarehe 20 Agosti, 2024 katika Ofisi za
Wizara Mtumba, jijini Dodoma.
xxxxxxxxxxxxxxxxxxx
Na
Hyasinta Kissima – WyKS
Waziri wa Katiba na Sheria
Mhe. Prof. Palamagamba Kabudi (Mb) ameanza kazi rasmi kwa kuwataka Watumishi wa
Wizara hiyo kuwa kinara katika kutekeleza kwa vitendo falsafa ya 4R ya Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Prof. Kabudi ameyasema hayo
tarehe 20 Agosti, 2024 wakati akizungumza na Watumishi katika hafla fupi ya
makabidhiano ya Ofisi yaliyofanyika Ofisi za Wizara Mtumba jijini Dodoma.
"Tunapozungumzia 4R za
Rais Samia Reconciliation (maridhiano), Reforms (mabadiliko), Resilience
(ustahimilivu) na Rebuilding (kujenga upya) sisi tunapaswa kuwa kinara.
Tunapozungumzia Reconciliation hatuangalii makundi ya Kisiasa pekee. Wapo
Wakulima na Wafugaji ambao nao wanahitaji upatanisho.Yapo mambo ya kijamii, uchumi,
utamaduni ambayo yanahitaji upatanisho. Tunapokwenda kutoa Msaada wa Kisheria
tunapatanisha watu, tunafanya usuluhishi, tunasaidia watu kuelewa haki zao. Tunafanya
Reform katika Sheria mbalimbali. Hivyo inatubidi kuhakikisha tunayasimamia haya
kikamilifu." Alisema.
Aidha, Waziri Kabudi amesema
kuwa anamshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu
Hassan kwa kuendelea kumwamini ambapo ameahidi kufanya kazi kwa bidii na kwa
uaminifu.
Akizungumza mara baada ya
kukabidhi Ofisi, Waziri wa Maliasili na Utalii ambaye ndiye aliyekuwa Waziri wa
Katiba na Sheria Mhe. Balozi Dkt. Pindi Chana alisema Wizara ya Katiba na
Sheria ilimpatia ushirikiano wa kutosha katika kuhakikisha anatimiza majukumu
yake ipasavyo na kuwataka watumishi waendeleze mshikamano huo kwa Prof. Kabudi
ambaye hii ni mara yake ya tatu kuongoza Wizara hiyo na amesema katika Wizara
ya Maliasili na Utalii yapo maeneo mengi ambayo Wizara hiyo inashirikiana na
Wizara ya Katiba na Sheria hususan katika kusimamia Haki za Binadamu.
Comments
Post a Comment