KATIBA NA SHERIA NA UONGOZI WA TLS WAKUBALIANA KUSHIRIKIANA
Katibu Mkuu Wizara ya Katiba na Sheria Bw. Eliakim Maswi
akiongoza majadiliano ya wataalam baina na Menejimenti ya Wizara na Uongozi wa
TLS kabla ya kumkaribisha Waziri wa Katiba na Sheria. 17/09/2024.
Baadhi ya viongozi kutoka Baraza la Uongozi la Chama cha
Mawakili wa Tanzania (TLS) wakifuatilia majadiliano katika kikao hicho. 17/09/2024.
Menejimenti ya Wizara na Uongozi wa TLS waliohudhuria katika kikao hicho wakifuatilia majadiliano. 17/09/2024.
Waziri wa Katiba na Sheria, Menejimenti ya Wizara na
Uongozi wa TLS wakiwa katika picha ya pamoja. 17/09/2024.
xxxxxxxxxxxxxxxxx
Na
Lusajo Mwakabuku & Hyasinta Kissima – WyKS Dodoma
Baraza la Uongozi la Chama cha
Mawakili wa Tanzania (TLS) likiongozwa na Rais wa Chama hicho Bw. Boniface
Mwabukusi wamekubaliana kwa pamoja na Wizara ya Katiba na Sheria chini ya
Waziri mwenye dhamana Mhe. Prof. Palamagamba John Kabudi kushirikiana katika
utekelezaji wa majukumu yote yanayohusu sekta ya sheria kwa kuzingatia mipaka
na taratibu kwa maslahi mapana ya Taifa.
Makubaliano hayo yamefikiwa
baada ya kikao cha majadiliano kilichofanyika kwa zaidi ya saa sita katika ukumbi
wa mikutano wa Makao Makuu ya Wizara yaliyopo Mtumba Jijini Dodoma tarehe
17/09/2024 na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali kutoka TLS huku Wizara ya
Katiba na Sheria ikiwakilishwa na Waziri wa Katiba na Sheria na Menejiment yote
ya Wizara.
Katika kikao hicho hoja
mbalimbali ziliibuliwa na kutokana na uzito wa majadiliano hayo, Waziri Kabudi
alielekeza Baraza hilo la TLS likae kwanza na Menejimenti ya Wizara ikiongozwa
na Katibu Mkuu bwana Eliakim Maswi kwa lengo la kujadili masuala ya kitaalamu
na baada ya hapo ikafuatia awamu ya pili iliyomjumuisha Waziri.
Hoja mbalimbali ziliibuliwa
katika kikao hicho moja wapo ikiwemo utekelezaji wa Kampeni ya Msaada wa
Kisheria ya Mama Samia (Mama Samia Legal Aid Campaign – MSLAC) ambapo TLS
waliitaka Wizara iwahusishe wanachama wengi zaidi wa TLS waliopo katika maeneo
mbalimbali nchini lengo likiwa ni kuwa na mwendelezo wa huduma mara kampeni
inapomalizika eneo husika. Waziri Kabudi alikubali ombi hilo na kuagiza iundwe Kamati
ya pamoja itakayojumuisha wanachama wa TLS na kuangalia namna bora zaidi ya
kuboresha utekelezaji wa kampeni hiyo.
Aidha jambo la pili
lililojadiliwa ni pamoja na uanzishwaji wa Kituo cha Kimataifa cha Usuluhishi
(Arbitration Center) ambachokitakuwa chombo cha kimataifa ambacho kitaweza
kuhudumia watu wa nchini na kutoka mataifa mbalimbali. Na hili pia Waziri
akaelekeza iundwe kamati na uandaliwe mpango mzuri juu ya uanzishwaji wa kituo
hiki.
Katika hatua nyingine, Rais wa
Chama hicho Bw. Mwabukusi akaiomba Wizara kupitia Taasisi zake hasa Tume ya
Kurekebisha Sheria kuhakikisha kuwa TLS inashirikishwa katika kutoa maoni
katika miswada mbalimbali kabla ya kufanywa kuwa sheria lengo ni katika
kuhakikisha kunakuwa na sheria bora zaidi za kusaidia wananchi. Jambo ambalo
Waziri Kabudi, kama ambavyo alikubali hoja zingine na hiyo aliikubali.
Akiongea mara baada ya
kukamilika kwa kikao hicho, Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Prof. Palamagamba
John Kabudi alisema anaamini kuwa huu ni mwanzo mzuri kwani wamekuwa na kikao
kizuri chenye majadiliano marefu ya staha ambapo mambo mengi mazuri yenye
kustawisha demokrasia ya nchi na ustawi wa jamii kupitia sekta ya sheria
yamejadiliwa na kupatiwa ufumbuzi.
Kwa upande wake Rais wa TLS Bw.
Mwabukusi alisema amefarijika kwa kiasi kikubwa kwanza kwa mapokezi ya heshima
waliyopewa tangu Wizarani hapo na namna mjadala ulivyoendeshwa huku akisema huu
ni mwanzo mzuri na wanatumaini kwa kusikilizana huku basi masuala mbalimbali
yanayowahusu wananchi kisheria yatapatiwa ufumbuzi.
Hii ilikuwa ni ziara ya kwanza
ya Rais wa TLS Bw. Mwabukusi kufika Wizarani kwa lengo la kujitambulisha tangu
ateuliwe kushika nafasi hiyo mwezi uliopita lakini kuwasilisha hoja mbalimbali
za kiutendaji ambazo anadhani ni muhimu TLS na Wizara wakashirikiana.
Comments
Post a Comment