WAZIRI KABUDI AHIMIZA USHIRIKIANO KWA TAASISI ZINAZOSIMAMIA HAKI JINAI


 Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Prof. Palamagamba John Kabudi akizungumza na Menejimenti ya Taasisi zinazounda Utatu wakati akifungua kikao cha Utatu Oktoba 9, 2024 jijini Dodoma.

Mkurugenzi wa Mashtaka nchini Bw. Sylvester Mwakitalu akizungumza katika kikao cha Utatu, 10 Oktoba, 2024 Jijini Dodoma.

Baadhi ya Wakuu wa  Taasisi zinazounda Utatu pamoja na Wakuu wa Mashtaka Mikoa, Wakuu wa Upelelezi Mikoa na Wakuu wa TAKUKURU Mikoa wakifuatilia hotuba ya Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Prof. Palamagamba John Kabudi wakati akifungua kikao cha Umoja huo tarehe 9 na 10 Oktoba, 2024 Jijini Dodoma.


xxxxxxxxxxxxxxxxxxxxx

Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Prof. Palamagamba John Kabudi amezitaka taasisi zinazosimamia masuala ya Haki Jinai kuhakikisha kuwa wanasimamia  na kuendeleza umoja na mshikamano waliouanzisha unaojulikana kama Utatu, ili kuongeza weledi na ufanisi katika kulinda Haki za watu wote kwa kufuata misingi ya Katiba na Sheria.

Waziri Kabudi amebainisha hayo tarehe 9 Oktoba, 2024 jijini Dodoma, wakati akifungua kikao cha Menejimenti ya taasisi zinazounda Utatu ikihusisha Menejimenti ya Ofisi ya Taifa ya Mashtaka, Ofisi ya Mkurugenzi  wa upelelezi wa Makosa ya Jinai na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Nchini kikao ambacho pia kilihudhuriwa na Wakuu wa Taasisi za Utatu kutoka Mikoa ya Tanzania Bara na Zanzibar.

Prof. Kabudi amesema kuwa Taasisi zinazosimamia Haki Jinai Nchini zinatakiwa kuendelea kutekeleza mapendekezo ya Tume ya Haki Jinai iliyoundwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ili kuhakikisha kuwa Wananchi wanapata Haki zao kwa wakati ikiwa ni pamoja na kufanya kazi kwa weledi, kuzingatia misingi ya haki ili kuhakikisha amani, utulivu na umoja vinametamalaki kwa maendeleo ya Nchi.

"Nikiangalia ushiriki wa Viongozi katika ngazi zote ni ishara kwamba mnathamini dhamana ambayo mmepewa. Kazi hii mnayoifanya kupeleleza, kuchunguza, kuendesha mashauri ya Jinai Nchini pamoja na kuwa na ushirikiano huu kwa ajili ya kutathmini mafanikio na changamoto zinazowakabili na namna ya kuzipatia ufumbuzi na kwa sasa tunapojiandaa kuelekea katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa na Uchaguzi Mkuu mwakani niwaombe mkasimamie Sheria zinazoongoza katika utendaji wenu ipasavyo  ili kuhakikisha umoja wa Nchi yetu, usalama wa Nchi yetu amani ya Nchi yetu vinaendelea kuwepo." Alisema Kabudi.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Mashtaka nchini Bw. Sylvester Mwakitalu amesema umoja huo wa Utatu uliundwa kwa lengo la kurahisisha utendaji wao wa kazi na pia kutatua changamoto wanazokumbana nazo wakati wa utekelezaji wa majukumu yao ambazo kwa namna moja ama nyingine zinachelewesha ama kukwamisha haki za watu.

"Tuliamua kila mwaka tuwe tunakutana Menejimenti ya Utatu na Viongozi wa ngazi za mikoa ili kujadiliana na kutathmini yale ambayo tumeyafanya pamoja na kuweka mikakati ya mwaka mwingine unaokuja, na tumekuwa na mijadala mizuri, mawasiliano na mada mbalimbali na kuongeza ufanisi katika majukumu yetu". Amefafanua hayo Mkurugenzi DPP.

 

Naye pia Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai Kamishna Ramadhani Kingai amesema ushirikiano wao umeleta manufaa makubwa kwao katika utekelezaji wa utoaji haki  katika jukwaa la haki jinai.

"Ni rai yangu kuendeleza na kuimarisha ushirikiano huu hususan katika kushughulikia makosa yanayovuka mipaka hivyo ni muhimu kukuza ushirikiano huu sio tu kwa Taasisi zetu bali pia taasisi nyingine za ndani na nje ya nchi." Amebainisha hayo DCI Kingai.

Sambamba na hilo Mkurugenzi wa Mashtaka Zanzibar Bw. Mgeni Jailan Jecha ametoa pongezi na shukrani kwa Menejimenti ya Bara kwa mwaliko wa ushiriki katika kikao hicho cha Utatu kwani kutasaidia kuzidi  kuimairisha mashirikiano ya sekta za Jinai baina ya Bara na Zanzibar, pia kujifunza na kupata uzoefu wa utendaji na kuchukua yale ambayo yatatokana na kikao hicho cha Utatu.


Comments

Popular posts from this blog

USAJILI WA VIZAZI NA VIFO NI TAKWA LA KISHERIA

TUFANYE KAZI KWA UADILIFU NA USHIRIKIANO - MHE CHANA