WATOA HUDUMA ZA MSAADA WA KISHERIA MSLAC LINDI WAPATIWA MAFUNZO

 

Mkurugenzi Idara ya Msaada wa Kisheria Bi. Ester Msambazi akizungumza na Wananchi wa Ruangwa Mkoani Lindi kupitia Redio Ruangwa ikiwa ni sehemu ya kutoa elimu ya Kampeni ya Msaada wa Kisheria ya Mama Samia na kuhamasisha Wananchi wa Mkoa wa Lindi kujitokeza katika uzinduzi wa Kampeni ya Msaada wa Kisheria tarehe 19 Februari, 2025 Mkoani Lindi.

xxxxxxxxxxxxxxx

Wizara ya Katiba na Sheria imeendesha kikao cha mafunzo kwa Wataalam watakaoshiriki katika utoaji wa huduma ya msaada wa kisheria Mkoani Lindi kupitia Kampeni ya Msaada wa Kisheria ya Mama Samia (Mama Samia Legal Aid Campaign) yenye lengo la kutoa elimu mbalimbali za Kisheria pamoja na utatuzi wa migogoro.

Akifungua kikao hicho kwa niaba ya Katibu Tawala Mkoa wa Lindi, Bwana. Nathalis Linuma ametoa rai kwa washiriki wa kikao hicho kuzingatia na kutumia mafunzo hayo kama chachu na mwangaza wa kuwasaidia wananchi kwa kuwapatia huduma za msaada wa kisheria katika kipindi cha kampeni.

"Ni matarajio yangu kuwa mtafuata mwongozo wa utekelezaji wa Kampeni ya Msaada wa Kisheria ya Mama Samia utakaotolewa na wataalam wa Wizara ili kuhakikisha kampeni inawanufaisha walengwa hususan wananchi wasio na uwezo wa kumudu gharama za Mawakili, ni vyema kuhakikisha kila mwananchi anaguswa na kampeni hii ili kwa pamoja tuweze kupunguza na kuondoa migogoro hususan ya kisheria inayowakabili wananchi"

Aidha, Bw. Linuma amewataka wananchi kujitokeza kwa wingi katika maeneo ya mikutano ili waweze kupata fursa ya kujifunza kuhusu masuala ya kisheria na kupata nafasi ya kuwasilisha mashauri yao ya kisheria ili kupata ufumbuzi na utatuzi wa shauri husika kwa usahihi.

Kwa upande wake Mkurugenzi na Msajiri wa Watoa Huduma za Kisheria Bi. Ester Msambazi  ameeleza kuwa Kampeni hii inatekelezwa katika Mikoa  26 yaTanzania bara na 5 ya Tanzania Zanzibar ambapo kati ya hiyo Mikoa 17 tayari imeshafikiwa.

"Uwepo wa kampeni hii umetokana na ombwe kubwa la kisheria lililopo miongoni mwa wanajamii hivyo kampeni imekuja kuleta uelewa wa masuala ya kisheria na elimu ya sheria miongoni mwa wananchi pamoja na kutoa huduma ya msaada wa kisheria inayohusu usuluhishi na utatuzi wa migogoro ikiwemo ya ardhi, jinai na madai pamoja na masuala ya mirathi na wosia"

Msaidizi wa Jeshi la Polisi na Mkuu wa Dawati la Jinsia na Watoto Mkoa wa Lindi, Joyce Kitesho ameeleza kuwa wanatarajia kampeni hii itakua ni chachu ya kupunguza migogoro mingi inayotokana na ukatili wa kijinsia ambayo waathirika wake wakuu ni wanawake na watoto.




Comments

Popular posts from this blog

USAJILI WA VIZAZI NA VIFO NI TAKWA LA KISHERIA

UONGOZI WA MAHAKAMA YA AFRIKA YA HAKI ZA BINADAMU NA WATU YAKUTANA NA VIONGOZI WA WIZARA YA KATIBA NA SHERIA

BODI YA KITAIFA YA USHAURI YA MSAADA WA KISHERIA YATEMBELEA WASAIDIZI WA KISHERIA IRINGA